


Na Mwandishi wetu,Morogoro
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) , Dkt. Adam Fimbo, ametoa pongezi kwa wajumbe wa Baraza la Sita la Wafanyakazi wa TMD kufuatia muda wake wa kuhudumu kufikia kikomo.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Kikao cha mwisho cha Baraza hilo la Wafanyakazi lililofanyika 5 Februari, 2026 mkoani Morogoro, Dkt. Fimbo amesema kuwa Baraza la Sita la wafanyakazi ambalo limedumu kwa miaka mitano limekuwa na mchango mkubwa katika mafanikio ya TMDA katika kipindi hiki ambayo yametokana na mahusiano mazuri baina ya uongozi na wafanyakazi kupitia ushirikishwaji wa wafanyakazi kwenye maamuzi makubwa yenye kuleta tija kwa taasisi kupitia vikao mbalimbali vya baraza.
Dkt . Fimbo amesema, katika kipindi cha baraza hili, mafanikio makubwa ya yaliyopatikana ndani ya TMDA ni pamoja na; kukamilika kwa jengo la ofisi ya TMDA Makao Makuu, Dodoma, kukamilika kwa nyumba za taasisi katika vituo vya mipaka vya Namanga na Tarakea na Ujenzi wa Tanuru la kuteketeza bidhaa duni na bandia kwa lengo la kulinda Afya ya Jamii.
Aidha, Dkt. Fimbo ameongeza kuwa mafanikio mengine ambayo Baraza hili linalomaliza muda wake limehusika nayo ni pamoja na TMDA kufikia ngazi ya 3 ya ukomavu ya WHO (WHO ML3) na kuiweka Tanzania kuwa nchi ya kwanza barani Afrika kufikia hadhi hiyo; Maabara kutambuliwa na WHO kuwa miongoni mwa Maabara bora duniani. Aidha, TMDA imeteuliwa na WHO kuwa Kituo cha Umahiri cha udhibiti wa dawa, chanjo na utoaji mafunzo ya kiudhibiti barani Afrika.
Pia, Baraza hili la Sita limekuwa na mchango katika kuhakikisha TMDA inaweka mazingira mazuri ya uanzishaji na uendelezaji wa viwanda vya dawa za binadamu 19, dawa za mifugo 2 na vifaa tiba 41 nchini, amesema Dkt. Fimbo
Naye mwakilishi wa Ofisi ya TUGHE Makao Makuu, Wkl. Mwanaidi Mgowa amepongeza uongozi wa TMDA kwa kuwa na Baraza la Wafanyakazi la mfano wa kuigwa na Mabaraza mengine. Aidha, Wkl. Mgowa ametoa wito kwa wajumbe wa TUGHE kujitokeza kwa wingi kushiriki katika uchaguzi ngazi ya Mkoa na Taifa utakaofanyika ndani ya mwaka 2026.
Akitoa salamu za Kamishna wa kazi, Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano, Bw. Peter Sembuyagi ameupongeza uongozi wa TMDA kwa kufikia mafanikio makubwa ambayo yamepatikana kupitia dhana ya ushirikishaji ambalo ni takwa la kisheria mahala pa kazi.
Baraza la Wafanyakazi la TMDA hudumu kwa kipindi cha miaka mitano na linaundwa na Menejimenti, wajumbe wa TUGHE na wawakilishi kutoka katika ofisi zote za Kanda ambapo hukutana mara mbili kwa mwaka kwa lengo la kujadili masuala makubwa ya kitaasisi ikiwa ni njia moja wapo ya ushirikishaji wa watumishi katika ngazi ya maamuzi.

























