INEC yaitaka jamii kuhamasisha amani na ushiriki katika uchaguzi Mkuu




Published from Blogger Prime Android App


Na Waandishi Wetu, Dar es Salaam

Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) imeyataka makundi mbalimbali ya kijamii nchini kuyatumia majukwaa yao kuwahamasisha wananchi kushiriki kwa wingi katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.
Wito huo umetolewa leo, tarehe 31 Julai 2025, jijini Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Tume hiyo,Mheshimiwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Jacobs Mwambegele, wakati akifungua mkutano kati ya Tume na wawakilishi wa watu wenye ulemavu.
Katika hotuba yake, Jaji Mwambegele ameeleza kuwa Tume inatambua na kuthamini mchango wa watu wenye ulemavu katika kueneza taarifa sahihi na kuhamasisha ushiriki wa wananchi katika uchaguzi.
“Nawasihi kutumia majukwaa yenu kuhimiza wenzenu kushiriki kwa amani na kuepuka kauli au vitendo vinavyoweza kuhatarisha utulivu wa nchi yetu wakati wa kampeni,” amesema Mhe. Mwambegele, na kuongeza kuwa Tume itaendelea kushirikiana nao katika hatua zote muhimu kuelekea uchaguzi.
Akizungumzia maandalizi ya uchaguzi mkuu, Jaji Mwambegele amesema kuwa ratiba rasmi imeshatangazwa ambapo utoaji wa fomu za uteuzi kwa wagombea wa nafasi mbalimbali utafanyika kuanzia tarehe 9 Agosti hadi 27 Agosti 2025, huku kampeni zikipangwa kuanza tarehe 28 Agosti
hadi 28 Oktoba 2025 kwa upande wa Tanzania Bara.
Katika mkutano mwingine na wawakilishi
wa wanawake uliofanyika pia jijini Dar es Salaam, Makamu Mwenyekiti wa Tume, Mheshimiwa Jaji wa Mahakama ya Rufani (Mstaafu) Mbarouk Salim Mbarouk, amewahimiza wanawake kutumia nafasi zao kuwafikishia wananchi taarifa sahihi kuhusu hatua
za maandalizi ya Uchaguzi Mkuu, na kuhamasisha waliojiandikisha kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kujitokeza kwa wingi siku ya kupiga kura.
Aidha, Jaji Mbarouk ametoa pongezi kwa wanawake kwa ushirikiano mkubwa waliouonyesha katika kipindi chote cha uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kilichoanza tarehe 20 Julai 2024 na kukamilika tarehe 4 Julai 2025.
"Natoa pongezi kwenu kwa namna mlivyotuunga mkono wakati wote wa zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la wapiga Kura. Tunawapongeza na tunawashukuru sana,” alisema Jaji Mbarouk.
Kwa upande wake, Mjumbe wa Tume, Mheshimiwa Jaji wa Mahakama Kuu Asina Omari, amewahimiza vijana kutumia mitandao ya kijamii kwa uadilifu, hasa kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi.
“Natoa wito kwenu kuwahamasisha vijana kuhusu matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii na kuepuka mitandao inayosambaza habari za chuki na uchochezi,” amesema Jaji Asina
Ameonya pia dhidi ya matumizi mabaya ya teknolojia ya akiliunde (AI), ambayo kwa sasa inatumika kusambaza taarifa za upotoshaji na chuki.
“Vilevile, muwakumbushe vijana wenzenu kuepuka matumizi mabaya ya akiliunde. Vijana ni kundi lenye nguvu, na mkitambua nafasi yenu, mtaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa katika kufanikisha uchaguzi mkuu wa mwaka huu,” aliongeza
Katika mikutano yote hiyo, viongozi wa Tume wamekumbusha kuwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 utafanyika kwa mujibu wa sheria mbili mpya zilizopitishwa mwaka 2024, ambazo zimeleta maboresho ya kiutendaji, kisheria na kiuwazi katika mchakato mzima wa uchaguzi.


Share:

DKT.BITEKO:TUNAWEZA KUZUIA ASILIMIA 80 YA VIFO NCHINI TUKIBADILI MTINDO WA MAISHA

Published from Blogger Prime Android App



📌 *Asisitiza kuhusu mazoezi ya mwili ili kujikinga na maradhi yasiyoambukiza*

📌 *Apongeza NBC Dodoma Marathon kuiunga mkono Serikali  mapambano dhidi ya Saratani ya Shingo ya kizazi na kusomesha Wataalam wa Afya*

📌 *Apongeza Kampeni ya MTU NI AFYA inayohamasisha Watanzania kufanya mazoezi*

📌 *NBC Dodoma Marathon yawezesha matibabu ya Saratani ya Shingo ya Kizazi kwa Wanawake 4800; mafunzo kwa Wakunga 100 na kuchangia ujenzi wa wodi*

Na Ofisi ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko amesema kuwa asilimia 80 ya vifo nchini vinaweza kuzuilika endapo Watanzania wataamua kubadili mtindo wa maisha ikiwemo  kuwa na utaratibu wa kufanya mazoezi ya mara kwa mara.
 
Amesema hayo tarehe 27 Julai, 2025 jijini Dodoma wakati akimwakilisha Waziri Mkuu, Mhe. Kassim Majaliwa katika kilele cha msimu wa Sita wa NBC Dodoma Marathon 2025 ambayo imelenga kukusanya fedha kwa ajili ya kuokoa afya ya mama na mtoto.

“Taarifa ya Shirika la Afya Duniani ya mwaka 2022, inaeleza kuwa, mazoezi ya mara kwa mara kama vile kukimbia, yana uwezo wa kupunguza hatari ya ugonjwa wa moyo kwa zaidi ya asilimia 35.Vile vile, mazoezi ya mwili husaidia kujikinga na magonjwa mengine yasiyoambukiza kama vile kisukari, shinikizo la damu, saratani na magonjwa mengine mengi.” Ameeleza Dkt. Biteko

Kwa upande wa Tanzania, Dkt. Biteko amesema kuwa asilimia 33 ya Watanzania watu wazima wana uzito uliopitiliza na asilimia 28 wana shinikizo la damu ambapo ameeleza kuwa magonjwa hayo yanachangia zaidi ya asilimia 40 ya vifo vya mapema lakini asilimia 80 ya vifo hivyo vinaweza kuzuilika kwa kubadili mtindo wa maisha.   
   
Dkt. Biteko ameipongeza Benki ya NBC kupitia NBC Dodoma Marathon kwa kuunga mkono Serikali katika nyanja mbalimbali ikiwemo Sekta ya Afya kwani katika mwaka 2025 Marathon hiyo imelenga kuendeleza mapambano dhidi ya Saratani ya shingo ya kizazi kwa kushirikiana na  Taasisi ya Saratani ya Ocean Road.

Pia, imelenga kutoa ufadhili wa masomo ya Wakunga kupitia Taasisi ya Benjamin Mkapa ili kusaidia kupunguza vifo vya mama na mtoto wakati wa uzazi na kutoa ufadhili kwa mafunzo ya Wauguzi  Maalum wa kusaidia watoto wenye changamoto ya usonji (Autism), kwa kushirikiana na AMREF Afrika.

 Vilevile, Dkt. Biteko amesema kuwa tangu NBC Dodoma Marathon kuanzishwa mwaka 2020 imekuwa ni moja ya vilelezo vya  kujenga mshikamano, uzalendo wa kweli na kutatua matatizo mbalimbali katika jamii ikiwemo changamoto za kiafya. 

Dkt. Biteko ameipongeza NBC Dodoma Marathon kwa kuendelea kuimarika kwani mwaka 2024 ilihusisha washiriki 8,000 na mwaka huu imekuwa na  washiriki zaidi ya 12,000 sawa na ongezeko la zaidi ya asilimia 50. 

Vile vile, mwaka 2024 NBC Dodoma Marathon ilikusanya kiasi cha Shilingi Milioni 300 huku mwaka 2025 ikikusanya kiasi cha Shilingi Milioni 700 sawa na ongezeko la mapato ya zaidi ya asilimia 133.33.

Amesema kuwa, Serikali itaendelea kushirikiana na wadau kama NBC ambao wameendelea kutumia mashindano ya mbio kuimarisha afya za wananchi na kuchangia masuala mbalimbali ya kijamii ikiwemo kuokoa afya za watu.

 Katika hatua nyingine, Dkt. Biteko ametoa rai kwa Wizara ya Afya, Serikali za Mitaa, Mashirika ya kiraia, Sekta binafsi na wananchi wote  kufanya mbio na mazoezi kuwa sehemu ya maisha ya kila siku ili kuweza kujikinga na matatizo ya afya ambayo wananchi wanaweza kuyapata.

“Nitashukuru sana kusikia kila Taasisi imetenga kwa uchache siku moja kwa mwezi ili kuwa na mazoezi ya pamoja, hii itasaidia kuimarisha afya zetu na kujenga Taifa Imara. “ Amesisitiza Dkt.Biteko     
 
Vilevile ameipongeza  Wizara ya Afya,  kwa Kampeni ya MTU NI AFYA ambayo inawahamasisha Watanzania kufanya mazoezi kwa angalau dakika 30 kila siku, kula lishe bora, kupima afya mara kwa mara na kujiepusha na tabia hatarishi.

Kwa upande wake, Mhe. Profesa Palamagamba Kabudi, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo amesema mbio za NBC Dodoma Marathon zimekuwa kivutio kwa wanamichezo wengi kushiriki kutokana na kundaliwa vizuri ambapo amesema kuwa Wizara hiyo itaendelea kuiunga mkono benki ya NBC katika maandalizi ya mbio hizo ambazo zimekuwa na matokeo chanya.

Amesema Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo itaendelea kuweka mazingira mazuri ya wananchi kushiriki michezo mbalimbali pamoja na kuendelea kujenga viwanja vya michezo katika maeneo mbalimbali ikiwemo Arusha, Dodoma na Dar es Salama ili kuwezesha vijana kujiimarisha kimichezo na kiafya.

 Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC, Theobald Sabi alisema NBC Marathon imekuwa ni moja ya alama za sekta binafsi katika kuwekeza kwenye sekta ya afya  na nyinginezo, akieleza kuwa katika kipindi cha miaka mitano mbio hizo zimefanikiwa kukusanya zaidi ya shilingi bilioni 1, ambazo zimekuwa na mchango mkubwa katika Sekta ya Afya.

Ametaja mafanikio ya marathon hiyo kuwa ni pamoja na kutoa elimu na kufanikisha kupimwa Saratani ya shingo ya kizazi kwa Wanawake zaidi ya 200,000 na kufadhili matibabu kwa wagonjwa 4,800 waliogunduliwa na kansa hiyo katika Hospitali ya Ocean Road.

Amesema, NBC Dodoma Marathon imetoa ufadhili kwa Wakunga 100 katika chuo cha Wakunga Morogoro kwa ushirikiano na Taasisi ya Benjamin Mkapa Foundation huku  lengo likiwa ni kufadhili wakunga 500 ifikapo 2028.

Pia ameeleza kuwa, NBC Dodoma Marathon imechangia ujenzi wa Wodi maalum ya Wanawake katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na maeneo mengine katika maendeleo ya sekta ya afya. 

Amesema msimu wa sita wa NBC Dodoma Marathon umehusisha wakimbiaji 12,000 na wamefanikiwa kukusanya shilingi milioni 700 kwa ajili ya afya ya mama na mtoto ikilenga  kuwapatia uchunguzi wa mwanzo wa saratani ya kansa ya kizazi wanawake 10,000, kutoa ufadhili kwa wakunga 100 na kuanzisha mpango mpya wa masomo kwa wauguzi 100 watakaoshughulika na watoto wenye changamoto ya usonji.  

NBC Dodoma Marathon 2025 iliyokuwa na kaulimbiu ya Kata Wese Okoa Maisha imehusisha wanariadha kutoka ndani na nje ya nchi ambapo washindi wamepewa zawadi za jumla ya shilingi milioni 80. Aidha imekabidhi pikipiki 10 kwa Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma.
Share:

RAIS SAMIA ATOA BILIONI NNE UJENZI KIWANDA CHA KUZALISHA NISHATI MBADALA

Published from Blogger Prime Android App



📌Kiwanda kuongeza uzalishaji na upatikanaji wa nishati safi nchini

📌REA kugharamia ununuzi wa mtambo wa STAMICO

📌Stamico yapania kusambaza Nishati Safi ya Rafiki Briquettes kila kona


Na Mwandishi wetu,DAR ES SALAAM

Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) pamoja na Shirika la Taifa la Madini (STAMICO) leo tarehe 22 Julai, 2025 wamesaini mkataba wenye lengo la kujenga kiwanda kipya cha kuzalisha nishati mbadala (Mkaa mbadala wa Rafiki Briquettes) mkoani Geita ambapo mkataba huo una thamani ya shilingi bilioni 4.5.

Katika hafla iliyofanyika katika Ofisi ndogo ya REA, Jijini, Dar es Salaam, REA itatoa jumla ya shilingi bilioni tatu na STAMICO itatoa shilingi bilioni 1.5; kwa mchanganuo huo, REA itagharamia ununuzi wa mtambo wakati STAMICO italipia upatikanaji wa kiwanja, ujenzi wa jengo la kiwanda na gharama za ufungaji wa mitambo. 

Mkataba huo umesainiwa na Mhandisi, Hassan Saidy, Mkurugenzi Mkuu wa REA pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO, Dkt. Venance Mwasse.

Mkataba huo utaifanya STAMICO kuwa na viwanda vikubwa vitano vya kuzalisha mkaa mbadala wa Rafiki Briquettes; viwanda vingine ambavyo vinaendelea na uzalishaji wa mkaa mbadala vipo wilaya ya Kisarawe mkoa wa Pwani, Kiwira mkoani Songwe, na viwanda vingine viwili vipo mkoani Dodoma na Tabora ambapo vipo kwenye hatua za mwisho za ukamilishwaji kabla kuanza uzalishaji. 

Akizungumza  katika hafla hiyo, Mhandisi, Hassan Saidy, amesema kuwa Wakala umepewa jukumu la kuhakikisha upatikanaji wa nishati safi ya kupikia unafikia asilimia 80 kwa Watanzania wote ifikapo mwaka 2034. 

“Katika kufanikisha lengo hilo, Wakala unatekeleza Miradi mbalimbali ikiwemo uwezeshaji katika kuongeza uzalishaji na usambazaji ili kuongeza upatikanaji wa nishati safi ya kupikia kwa Watu wa vijijini.”

“Utiaji wa saini wa Mkataba huo kati ya REA na STAMICO ni moja wapo ya utekelezaji wa maagizo ya Mheshiwa, Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Wakala ili kushirikiana na Shirika la Madini la Taifa kuona namna ya kuongeza uzalishaji na upatikanaji wa nishati safi kwa Wananchi ili waondokane na matumizi ya nishati zisizo safi na salama”. Amesema Mhandisi, Hassan Saidy, Mkurugenzi Mkuu REA.

“Ni matumaini yetu kuwa Mkataba huu utaende kuongeza kasi ya upatikaji wa mkaa mbadala na kwa bei nafuu ikiwa ni mojawapo ya lengo la Mkakati wa Nishati Safi ya Kupikia. Tunatambua kuwa utunzaji wa mtambo huu ni muhimu sana ili huduma iliyokusudiwa iendelee kutolewa kwa wakati bila kuathili uchumi wa Wananchi, afya na pamoja na mazingira kwa ujumla”. Amekaririwa, Mhandisi, Hassan Saidy.

Mhandisi, Saidy ameongeza kuwa Wakala unaendelea kushirikiana na Wadau mbalimbali ili kuhakikisha Mkakati wa Nishati safi ya kupikia unatimiza malengo yaliyowekwa, ikiwa ni pamoja na kuongeza upatikanaji na usambazaji wa mkaa mbadala, Wakala unaendelea kutekeleza Miradi mbalimbali ikiwemo usambazi wa majiko banifu, usambazaji wa majiko ya umeme, usambazaji wa mitungi ya gesi ya kupikia majumbani (LPG ya kilo 6 na 15); usambazaji wa gesi asilia katika mkoa wa Lindi na Pwani pamoja na ujenzi wa miundombinu ya nishati safi ya kupikia katika Taasisi za Umma. 

Kwa upande wake, Dkt. Venance Mwasse, Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO ameishukuru Serikali kupitia REA kwa mchango huu ambao utasaidia Shirika hilo  kutimiza ndoto yake ya kuhakikisha wananchi wote wanaachana na nishati isiyo safi na salama ya kupikia ifikapo mwaka 2034 na hivyo kuunga mkono juhudi za Serikali za kutunza mazingira. 

“Hii ajenda ya matumizi ya nishati safi ambayo kinara wake ni Rais wa Awamu ya Sita, Dkt. Samia Suluhu Hassan inalenga kumkomboa Mwanamke ili aachane na nishati isiyo safi na salama. STAMICO tumejipanga kutekeleza maono haya ya Kiongozi wetu”, amesema Dkt. Mwasse. 

Ameongeza kuwa nishati ya Rafiki Briquettes kwa sasa inatumiwa na Jeshi la Magereza ambapo Magereza yote 129 nchini kote yanatumia nishati hii kama aina mojawapo ya nishati ya kupikia, vikosi vya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) pamoja na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT). 

Taasisi nyingine ni pamoja na vyuo mbalimbali vya mafunzo, shule za msingi na sekondari, hoteli, migahawa, na sehemu wanazochoma nyama na chipsi. 

Dkt. Mwasse amesisitiza kuwa STAMICO itaendelea kutunza mitambo hiyo ili iendelee kutoa huduma kwa Wananchi
Share:

INEC YAHIMIZA viongozi wa siasa kufanya kampeni za kistaarabu

Published from Blogger Prime Android App


Na Mwandishi Wetu, DODOMA

Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) , imekutana na viongozi wa vyama vya siasa  kwa lengo la kujadiliana kuhusu maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, kubadilishana uzoefu, na kujenga uelewa wa pamoja wa mchakato wa uchaguzi.

Akizungumza jijini Dodoma leo Julai 27,2025 katika Makao Makuu ya INEC  na viongozi wa vyama vya siasa nchini,Mwenyekiti wa Tume, Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele, amesema kikao hicho kinalenga kuwapa wadau taarifa rasmi kuhusu maandalizi ya uchaguzi, na kusisitiza umuhimu wa kuzingatia ratiba rasmi na masharti ya kisheria, hususan wakati wa utoaji wa fomu na uteuzi wa wagombea.

Jaji Mwambegele alieleza kuwa Tume itazingatia Katiba, Sheria na Kanuni ili kuhakikisha kila mgombea mwenye sifa anapata haki ya kuteuliwa kwa kufuata utaratibu. Aidha, alivitaka vyama vya siasa kuendesha kampeni kwa amani na ustaarabu, akionya kuwa joto la kisiasa lisiposimamiwa linaweza kuhatarisha utulivu wa nchi.

Ameongeza kuwa Tume italinda usawa kwa vyama vyote kwa kuhakikisha kila chama kinapata fursa ya kunadi sera zake kwa mujibu wa ratiba rasmi.

Katika kuelekea uchaguzi huo, ametaja kuwa kutakuwa na jumla ya majimbo 272 ya uchaguzi, ambapo 222 yako Tanzania Bara na 50 Zanzibar, baada ya kuongezwa majimbo nane mapya Bara. Vilevile, kata zitakazoshiriki uchaguzi wa madiwani zimefikia 3,960 baada ya kuongezeka kwa kata tano mpya zilizoundwa na TAMISEMI.

Kwa mujibu wa ratiba, kampeni za uchaguzi zitafanyika kuanzia Agosti 28 hadi Oktoba 28 kwa Tanzania Bara, na hadi Oktoba 27 kwa Zanzibar. Katika kipindi hicho, wagombea na vyama vyao watatumia fursa hiyo kueleza sera na ilani kwa wananchi.

Naye Mkurugenzi wa Uchaguzi, Ramadhan Kailima, amesema maandalizi ya vifaa vya uchaguzi yanaendelea vizuri, na kwamba Tume imeweka utaratibu utakaowezesha wapiga kura waliotoa taarifa mapema kupiga kura ya urais katika vituo tofauti na walivyojiandikisha, ili kuhakikisha kila Mtanzania anapata haki ya kupiga kura.
Share:

INEC yazindua rasmi kalenda ya kampeni za uchaguzi Mkuu


Published from Blogger Prime Android App




Na Mwandishi wetu DODOMA

TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) imezindua rasmi  kalenda ya uchaguzi Mkuu huku ikitangaza ongezeko kubwa la idadi ya wapiga kura waliojiandikisha kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, ikiwa ni matokeo ya mafanikio ya zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa Tanzania Bara na Zanzibar.

Akizungumza jijini Dodoma katika hafla ya Uzinduzi huo, Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji wa Rufaa Jacobs Mwambegele, amesema jumla ya wapiga kura waliojiandikisha ni milioni 37.655 ikiwa ni ongezeko la asilimia 26.55% kutoka wapiga kura milioni  29.754 waliokuwepo mwaka 2020.

“Kati ya hao milioni 36.650 ni kutoka Tanzania Bara, huku Zanzibar ikiwa na wapiga kura milioni 1.0 Idadi hii inaonesha mwitikio chanya wa wananchi kushiriki katika mchakato wa kidemokrasia,” amesema Jaji Mwambegele.

Kwa upande wa Zanzibar, ilielezwa kuwa wapiga kura 725,876 wako katika Daftari la ZEC, huku wengine 278,751 wakiwa wameandikishwa na INEC baada ya kukosa sifa za kujiandikisha kupitia ZEC.

Ratiba ya Uchaguzi Mkuu 2025

Kwa mujibu wa mamlaka ya kikatiba na kisheria chini ya ibara ya 41(4) ya Katiba ya 1977, pamoja na Sheria ya Uchaguzi Na. 1 ya 2024, INEC imetangaza ratiba rasmi ya uchaguzi ambapo Agost 9 - 27, 2025 ni utoaji wa fomu za uteuzi wa wagombea wa Kiti cha Rais na Makamu wa Rais,Agosti 14 - 27, 2025 ni utoaji wa fomu za uteuzi wa wagombea wa Ubunge na Udiwani.

 Agosti 27 , 2025 ni siku ya Uteuzi wa wagombea wa nafasi zote,Agosti 28 hadi Oktoba 28 , 2025 ni kampeni za Uchaguzi kwa Tanzania Bara,Agosti hadi Ojtoba  27 , 2025 ni  Kampeni za Uchaguzi kwa Tanzania Zanzibar ili kupisha kura ya mapema na Oktoba 29, 2025 (Jumatano) itakuwa ni Siku rasmi ya Kupiga Kura.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Uchaguzi Ramadhan Kailima amekabidhi rasmi orodha ya watu 8,703 waliojiandikisha zaidi ya mara moja kwa Jeshi la Polisi. 

Taarifa hiyo ni sehemu ya kalenda ya uchaguzi, na hatua za kisheria zitaendelea kuchukuliwa kwa mujibu wa Kifungu 114 cha Sheria ya Uchaguzi, ambacho kinaainisha adhabu kwa makosa hayo.

Ametoa wito kwa wananchi na wadau wote kushiriki kikamilifu katika mchakato wa uchaguzi kwa kuzingatia sheria, kanuni, miongozo, na maelekezo yatakayotolewa na Tume katika kipindi chote kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.
Share:

Kumbukumbu ya Siku ya Mashujaa  Brigedia Jenerali Mstaafu Balozi Mndolwa atoa wito kwa Waandishi wa Habari kuwa Wazalendo



Published from Blogger Prime Android App




Na Joyce Kasiki

 MMOJA wa Mashujaa waliopigana vita ya Kagera Brigedia Jenerali mstaafu na Balozi Francis Mndolwa amewaasa  waandishi wa habari nchini kuandika habari zenye kuijenga jamii, kuleta heshima kwa Taifa, na kukuza uzalendo ikiwa ni sehemu ya ujenzi juhudi za mashujaa hao pamoja na waasisi wa Taifa la Tanzania.

Akizungumza na waandishi wa habari katika katika maadhimisho ya kumbukumbu ya Mashujaa nchini , Balozi Mndolwa aliwataka kuenzi kazi yao kama sehemu ya mchango mkubwa kwa Taifa.

"Waandishi muandike habari ambazo zitawainua na kuwaheshimisha. Waandishi wote wa habari mnapaswa kuwa wazalendo,nchi hii imetoka mbali, inahitaji msaada wa kila mmoja wenu ili tuendelee kuwa na amani.”

Balozi Mndolwa aliwakumbusha waandishi kuhusu historia ya taifa, akitaja jinsi viongozi waasisi kama Mwalimu Julius Nyerere na Mzee Abeid Amani Karume walivyoweka msingi wa mshikamano wa kitaifa, amani na maendeleo. 

Alisisitiza kuwa Tanzania imeweza kudumisha utulivu wa muda mrefu licha ya changamoto zinazozikumba nchi nyingi jirani.

"Nchi nyingi zinazotuzunguka zimebomoka, zimepata matatizo, lakini tuwashukuru taasisi zetu, Mwalimu Nyerere, Mzee Karume, kwa kuwaandaa wananchi ambao sasa wanaendelea na juhudi zao na nchi kuwa na amani,” amesema

Mndolwa pia alitoa wito kwa waandishi na Watanzania kwa ujumla kujiepusha na kuiga migogoro ya mataifa makubwa duniani.

"Msiwe na mwendo wa upinzani wa dunia, tunawaona Warusi, Wachina wakigombana na Marekani ,huo ni ugomvi wao wa dunia, hatuutaki. Tunataka hivi tulivyo, lazima tushirikiane,” aliongeza kwa msisitizo.

Maadhimisho ya Siku ya Mashujaa ni wakati wa kukumbuka na kuthamini mchango wa watetezi wa taifa waliopigania uhuru, usalama, na heshima ya nchi. 




---


Share:

Ivo Mapunda kuwa Kocha Mkuu wa timu ya Taifa ‘Tembo Warriors’. 



Published from Blogger Prime Android App


Na Mwandishi Wetu
SHIRIKISHO la Mpira wa Miguu kwa watu wenye ulemavu (TAFF) limetangaza Ivo Mapunda kuwa Kocha Mkuu wa timu ya Taifa ‘Tembo Warriors’. 
Katika taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Ufundi wa Taff, Shaban Msangi amesema atakuwa kocha kwa muda wa mwaka mmoja huku akitazamwa mafanikio yake.
Msangi alisema kutokana na Tembo Warriors kukabiliwa na michuano ya Afrika Mashariki na Kati (CECAAF) inayotarajiwa kufanyika Septemba mwaka huu Bujumbura, Burundi Jumatatu watakutana na Ivo Mapunda kupanga siku ya kutangaza kikosi cha timu ya Taifa.
Ivo Mapunda ambaye ni mchezaji wa zamani wa Simba, Yanga pamoja na timu ya Taifa ya soka ‘Taifa Stars’ alikuwa sehemu ya benchi la Tembo Warriors mwaka 2022 kama kocha wa magolikipa katika michuano ya Kombe la Dunia yaliyofanyika nchini Uturuki.
Share:

WAZIRI MKUU AMALIZA ZIARA BELARUS, ANADI FURSA ZA UWEKEZAJI NCHINI



Published from Blogger Prime Android App



Na Mwandishi Wetu

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa ametumia ziara yake nchini Belarus kunadi fursa za uwekezaji katika maeneo manne ya kipaumbele ya Serikali ya awamu ya sita ambayo ni kilimo, afya, madini na ulinzi & usalama.

Mhe. Waziri Mkuu katika siku mbili za ziara yake,  Julai 22 na 23 mwaka huu ametembelea kampuni kubwa nane zenye nguvu ya mitaji jijini Minsk na kuzihakikishia utayari wa Serikali ya Tanzania kushirikiana nazo kwa kuzipatia kila aina ya msaada zitakapokuja Tanzania kuwekeza.

Kwenye eneo la kilimo, Mhe. Waziri Mkuu alikutana na viongozi wa kampuni ya AFTRADE ambayo tayari ipo nchini na kuwasisitiza kuongeza kasi katika kuendeleza kilimo hususan kuwa na programu za kuwasaidia wakulima wadogo mitaji, utafiti na mafunzo ili kilimo  kiweze kuwa na tija, kizalishe ajira na kuongeza usalama wa chakula nchini.

Katika eneo hilo la kilimo, Waziri mkuu pia alitembelea chuo cha kilimo cha Belarus na viwanda vya matrekta na  kuvishawishi viwanda hivyo kufungua matawi nchini Tanzania. 

Kuhusu chuo cha kilimo ambacho mafunzo yake huyafanya kwa vitendo zaidi,  Waziri Mkuu aliomba Watanzania wapatiwe fursa za masomo katika chuo hicho ili waweze kuendeleza sekta ya kilimo nchini, watakapomaliza masomo yao.

Kuhusu Afya, Mhe. Waziri Mkuu alitembelea kampuni ya kuzalisha na kusambaza dawa na vifaa tiba ya Belmedepreparaty ambayo ni moja ya kampuni kubwa nchini Belarus. Kampuni hiyo inayozalisha bidhaa tofauti tofauti zaidi ya 1700 na kuuza ndani na nje ya nchi katika mataifa zaidi ya 24, iliridhia maombi ya Mhe. Waziri Mkuu na kuahidi kufanya ziara nchini Tanzania kuangalia fursa za uwekezaji.

Mhe. Waziri Mkuu alisema Belmedepreparaty ni kampuni sahihi kuja kuwekeza nchini kutokana na kutumia teknolojia ya kisasa ya kuzalisha bidhaa zenye ubora na viwango vya kimataifa.

Kwa upande wa sekta ya madini, Waziri Mkuu alitembelea kiwanda cha kutengeneza mitambo inayotumika kuchimba madini migodini na kukishawishi kiwanda hicho kuja kuwekeza nchini Tanzania. 

Kuhusu suala la Ulinzi na Usalama, Mhe. Waziri Mkuu alitembelea kiwanda cha kutengeneza vifaa vya ukoaji na kuzima moto na kusisitiza umuhimu wa kushirikiana na kiwanda hicho ili kuondoa tatizo la uhaba wa vifaa hivyo nchini.

Waziri Mkuu amemaliza ziara yake na aliondoka Julai 24, 2025 kurejea nyumbani.
Share:

*DKT. TULIA AFUNGUA KIKAO CHA JUKWAA LA KIBUNGE UN*




Published from Blogger Prime Android App



Na Mwandishi wetu

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Rais wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU), Mhe. Dkt. Tulia Ackson, leo tarehe 22 Julai 2025, amefungua rasmi Kikao cha Jukwaa la Kibunge katika Mkutano wa Ngazi ya Juu wa Umoja wa Mataifa wa Mwaka 2025 kuhusu Maendeleo Endelevu _(Parliamentary Forum at the 2025 UN High Level Political Forum on Sustainable Development)_, kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, New York, Marekani.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Mhe. Dkt. Tulia ameeleza umuhimu wa Mabunge duniani kushirikiana kwa karibu na Serikali zao katika kujenga mifumo imara ya usawa wa kijinsia na afya kwa wote, sambamba na utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs), hususani Lengo namba 3 (Afya kwa Wote) na Lengo namba 5 (Usawa wa Kijinsia).

Akigusia Lengo la 3, Dkt. Tulia ameeleza kuwa bado kuna pengo kubwa katika upatikanaji wa huduma bora za afya, hasa katika nchi zinazoendelea, licha ya kwamba malengo haya yanatarajiwa kufikiwa ifikapo mwaka 2030. Amehimiza haja ya ushirikiano madhubuti baina ya Serikali na Mabunge katika kuhakikisha kwamba huduma hizo zinaboreshwa na kufikika kwa wote.

Kuhusu Lengo la 5, Dkt. Tulia amesema licha ya mafanikio yanayoendelea kupatikana katika kupambana na ukatili, ubaguzi na ukosefu wa ushiriki wa wanawake katika siasa na uongozi, bado ipo kazi kubwa ya kufanya. Amesisitiza kuwa Mabunge yana wajibu wa kuendelea kutunga na kusimamia sheria zinazoimarisha haki, usawa, uwajibikaji na ufadhili wa kweli kwa mipango ya kuwawezesha wanawake na wasichana ili kufikia maendeleo jumuishi na endelevu.



























KT. TULIA AFUNGUA KIKAO CHA JUKWAA LA KIBUNGE UN*

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Rais wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU), Mhe. Dkt. Tulia Ackson, leo tarehe 22 Julai 2025, amefungua rasmi Kikao cha Jukwaa la Kibunge katika Mkutano wa Ngazi ya Juu wa Umoja wa Mataifa wa Mwaka 2025 kuhusu Maendeleo Endelevu _(Parliamentary Forum at the 2025 UN High Level Political Forum on Sustainable Development)_, kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, New York, Marekani.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Mhe. Dkt. Tulia ameeleza umuhimu wa Mabunge duniani kushirikiana kwa karibu na Serikali zao katika kujenga mifumo imara ya usawa wa kijinsia na afya kwa wote, sambamba na utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs), hususani Lengo namba 3 (Afya kwa Wote) na Lengo namba 5 (Usawa wa Kijinsia).

Akigusia Lengo la 3, Dkt. Tulia ameeleza kuwa bado kuna pengo kubwa katika upatikanaji wa huduma bora za afya, hasa katika nchi zinazoendelea, licha ya kwamba malengo haya yanatarajiwa kufikiwa ifikapo mwaka 2030. Amehimiza haja ya ushirikiano madhubuti baina ya Serikali na Mabunge katika kuhakikisha kwamba huduma hizo zinaboreshwa na kufikika kwa wote.

Kuhusu Lengo la 5, Dkt. Tulia amesema licha ya mafanikio yanayoendelea kupatikana katika kupambana na ukatili, ubaguzi na ukosefu wa ushiriki wa wanawake katika siasa na uongozi, bado ipo kazi kubwa ya kufanya. Amesisitiza kuwa Mabunge yana wajibu wa kuendelea kutunga na kusimamia sheria zinazoimarisha haki, usawa, uwajibikaji na ufadhili wa kweli kwa mipango ya kuwawezesha wanawake na wasichana ili kufikia maendeleo jumuishi na endelevu.
Share:

Watendaji wa uchaguzi watakiwa kutoa taarifa mapema




Published from Blogger Prime Android App



Na. Mwandishi wetu, Shinyanga
Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi imewataka watendaji wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 kutoa taarifa mapema kwa vyama vya siasa kuhusu utaratibu wa kuwaapisha mawakala.
 
Hayo yamesemwa mkoani Shinyanga leo Julai 21, 2025 na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jacobs Mwambegele wakati akifungua mafunzo kwa watendaji wa uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi oktoba mwaka huu kwa tarehe itakayotangazwa na Tume.
 
“Wakati wa kuapisha mawakala, toeni taarifa mapema kwa vyama vya siasa kwa mujibu wa sheria, kanuni na maelekezo ya Tume na kuvipatia vyama vya siasa orodha ya vituo vya kupigia kura ili kuviwezesha kupanga mawakala,” amesema Jaji Mwambegele.
 
Amewasisitiza watendaji hao kuhakikisha vifaa vya uchaguzi wanavyopokea kutoka Tume, wanavihakiki, kuvikagua na kuhakikisha vinasambazwa kwenye vituo vyote na kila mkuu wa kituo anapata vifaa vyote vya uchaguzi vinavyohitajika mapema.
 
Amewataka kuhakikisha kuwa siku ya uchaguzi wanaweka utaratibu utakaowezesha kila kituo cha kupigia kura kufunguliwa saa 1:00 kamili asubuhi na kufanya mawasiliano na Tume pale ambapo ushauri utahitajika kuhusiana na masuala ya uchaguzi.
 
Akifungua mafunzo kama hayo Kisiwani Pemba, Zanzibar, Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani (Mstaafu) Mbarouk Salim Mbarouk amewaasa watendaji hao kufanya kazi kwa kuzingatia Katiba, Sheria, Kanuni, miongozo na maelekezo mbalimbali yaliyotolewa na yatakayotolewa na Tume.
 
 “Jitahidini na mjiepushe kuwa vyanzo vya malalamiko kutoka kwa vyama vya siasa na wadau wa uchaguzi. Hakikisheni mnazingatia ipasavyo Katiba, Sheria, Kanuni, miongozo na maelekezo mbalimbali yaliyotolewa na yatakayotolewa na Tume,” amesema Jaji Mwambegele.
 
Amewataka kuwashirikisha wadau wa uchaguzi kwenye maeneo wanayopaswa kushirikishwa kwa mujibu wa Katiba, Sheria, Kanuni, miongozo na maelekezo ya Tume.
 
Amewakumbusha kuhusu wajibu wao wa kuhakikisha wanavitambua vituo vya kupigia kura mapema ili kubaini mahitaji maalum ya vituo husika na kuhakikisha kunakuwa na mpangilio mzuri ambao utaruhusu uchaguzi kufanyika kwa utulivu na amani.
 
“Ajira za watendaji wa vituo zizingatie kuajiri watendaji wenye weledi, wanaojitambua, wazalendo, waadilifu na wachapakazi na kuachana na upendeleo kwa ndugu na jamaa ambao hawana sifa za kufanya shughuli za uchaguzi,” amesema Jaji Mbarouk.
 
Mafunzo hayo yanafanyika kwa siku tatu kwenye mikoa mbalimbali nchini kwa siku tatu na yanawajumuisha waratibu wa uchaguzi, wasimamizi wa uchaguzi na wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi ngazi ya jimbo.

Tume imeyagawa mafunzo hayo kwenye awamu mbili ambapo awamu hii ya pili inahusisha mikoa ya Simiyu, Shinyanga, Kusini Pemba, Kaskazini Pemba, Mwanza, Mara, Dar es Salaam, Pwani, Rukwa, Katavi, Manyara, Arusha, Songwe na Mbeya.
 
Awamu ya kwanza ilifanyika tarehe 15 hadi 17 na ilihusisha watendaji kutoka mikoa ya Morogoro, Singida, Dodoma, Kaskazini Unguja, Kusini Unguja, Mjini Magharibi, Geita, Kagera, Mtwara, Lindi, Tabora, Kigoma, Tanga, Kilimanjaro, Ruvuma, Iringa na Njombe.
Share:

Hakuna mgombea aliyekatwa,CPA Makalla awatoa hofu wagombea CCM


Published from Blogger Prime Android App



Na Mwandishi wetu, Dodoma

KATIBU wa Itikadi ,Uenezi na Mafunzo  wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), CPA Amos Makalla, ametoa ufafanuzi kuhusu mchakato wa uteuzi wa wagombea wa nafasi za ubunge na udiwani, akisisitiza kuwa vikao muhimu vya maamuzi vitafanyika jijini Dodoma kuanzia Julai 26 hadi Julai 28, mwaka huu.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Julai 19,2025 Makao Makuu ya chama hicho  jijini Dodoma, Makalla alieleza kuwa kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) kitafanyika Julai 26 na kitatanguliwa na kikao cha Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya chama hicho  siku hiyo hiyo, ambapo maamuzi ya awali kuhusu mchakato wa uteuzi yatawekwa wazi.

Makalla amesema maandalizi ya uchaguzi ndani ya CCM yanaendelea vizuri, huku kikao cha mwisho kuhusu uteuzi wa wagombea kikiwa kimepangwa kufanyika Julai 28, mwaka huu  jijini Dodoma.
 
Amesema vikao hivi vya juu vitaamua majina ya wagombea watakaopeperusha bendera ya chama hicho kwenye uchaguzi ujao katika ngazi za Ubunge na udiwani.

"Leo wengi walitarajia Kamati Kuu ingeketi kwa ajili ya uteuzi, lakini shughuli hiyo sasa imepangwa kufanyika Julai 28. Hili ni zoezi nyeti linalohitaji umakini mkubwa, na ndiyo maana tumeamua kujipa muda zaidi ili tuweze kufanya kazi hii kwa weledi," amefafanua Makalla.

Aidha, Makalla amewataka wagombea wote waliowasilisha nia zao kuwa watulivu na kuvuta subira wakati mchakato ukiendelea, akibainisha kuwa jumla ya watu zaidi ya 10,000 wameomba ubunge, huku zaidi ya watu 27,000 wakitia nia kugombea nafasi ya  udiwani kupitia CCM.

"Napigiwa simu nyingi kuhusu lini uteuzi utafanyika. Sasa nawaambia, kazi ni kubwa, lakini tunaenda kwa hatua makini,hakuna mtu aliyekatwa bado, na kikao cha Julai 28 ndicho kitaamua rasmi nani anasonga mbele," amesisitiza.

Baada ya uteuzi huo, Makalla aliongeza kuwa chama kitapanga na kutangaza ratiba ya kura za maoni, hatua inayofuata katika mchakato wa kuwapata wagombea wa mwisho. 

Amesisitiza kuwa chama hakina shaka na tarehe iliyopangwa na kimejipanga kutoa wagombea bora na wa kuaminika.

CPA Makalla amewahimiza wagombea wote kuwa watulivu  hadi pale vikao vya mwisho vitakapotoa maamuzi rasmi kuhusu wagombea watakaoteuliwa kwenda kwenye kura za maoni.

Share:

TBN yaipongeza Serikali kwa mafunzo maalum kwa Mabloga kuelekea uchaguzi Mkuu




Published from Blogger Prime Android App


Na Mwandish wetu, Dar es Salaam.

CHAMA cha Mtandao wa Mabloga Tanzania (TBN) kimeshukuru uamuzi wa serikali ya kuwapatia mafunzo maalumu ya kunoa weledi na uzalendo wa wanachama wake kuelekea uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba mwaka huu. Mabloga zaidi ya 200 wakiwemo wa diaspora walioanzisha Mtandao huo mwaka 2015 watapata mafunzo hayo. 

“Tumekuwa na mazungumzo na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) ambao kimsingi ndio wasimamizi wakuu wa maudhui na wametuthibitishia kwamba wapo hatua za mwisho za kutekeleza maagizo ya serikali ya kutoa mafunzo kwa mabloga wote nchini,” alisema Mwenyekiti wa TBN , Beda Msimbe. 

Akifafanua kuhusu mafunzo hayo, Msimbe alisema kwamba lengo kuu la mafunzo ni kuwajengea mabloga weledi, uzalendo, na umakini katika kutambua na kupambana na habari feki, huku wakiwezesha usambazaji wa taarifa sahihi zitakazowawezesha wananchi kufanya maamuzi sahihi katika uchaguzi mkuu ujao. 

“ Tunahitaji kukumbushana kuhusu nchi hii, katiba yetu, amani na umuhimu wa uchaguzi katika demokrasia ya aina yetu.Uamuzi huu wa serikali wa kutupiga msasa ni muhimu sana” alifafanua.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari Mwenyekiti huyo wa TBN, Beda Msimbe, alieleza kuridhishwa na juhudi zinazofanywa na serikali kufanikisha mafunzo. Alisema wameomba mafunzo hayo kipindi cha sasa kwa kuwa wapo wanablogu ambao ni mara ya kwanza kuelekea katika uchaguzi mkuu, na kurejea ombi lao tena wakati wa mkutano wa wadau ulioandaliwa na Wizara ya Habari,Utamaduni,sanaa na michezo. 

Alisema kwamba uongozi wa TBN kwa sasa unafanya kazi kwa karibu na serikali kuhakikisha kuwa zaidi ya wanachama 150 wa chama hicho waliotawanyika nchini kote wanafaidika kikamilifu na mafunzo haya muhimu. 

Msimbe aliwataka mabloga wote nchini kuhakikisha wanawasiliana na Mratibu wa TBN, Bw. Gadiola Emanuel ili kuthibitisha anwani zao na kuhakikisha taarifa zao ziko sahihi kwa ajili ya ushiriki. Pia alitumia fursa hiyo kuwaalika wale wote ambao bado hawajajiunga na TBN kufanya hivyo sasa ili waweze kunufaika na fursa hii muhimu ya mafunzo. 

Chama cha Mabloga Tanzania (TBN) kinajumuisha mabloga wanaotengeneza aina mbalimbali za maudhui, ikiwemo michezo, habari za siasa, afya, uchumi, na habari mchanganyiko. Mafunzo haya yanatarajiwa kuimarisha uwezo wao wa kutoa taarifa zenye ukweli na uhakika, hivyo kuchangia katika mazingira ya uchaguzi yenye uwazi na uwajibikaji. 
Share:

Serikali kutoa mafunzo kwa waandishi wa blogu


Published from Blogger Prime Android App


Ns Mwandishi wetu


SERIKALI imekubali kutoa mafunzo maalum kwa waandishi wa blogu kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2025, hatua muhimu itakayowajengea uwezo na kuwaandaa kubeba dhamana kubwa ya usambazaji wa hbari sahihi.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wizara ya Habari,Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa katika Mkutamo wa Wadau Kujadili Mchango wa Sekta ya habari Katika kufanikisha uchaguzi Mkuu 2025.

Katika mkutano huo kipindi cha majadiliano Mwenyekiti wa Chama cha Mabloga Tanzania (TBN), Beda Msimbe, aliomba serikali kuona umuhimu wa kufunza mabloga wengi ambao sio waandishi lakini wanatengeneza maudhui kuwa na weledi kuandika masuala ya siasa kuelekea uchaguzi mkuu.

Akizungumza kwenye mkutano huo uliofanyika Mlimani City jijini Dar es Salaam, Julai 9, 2025, Bwana Msimbe alisisitiza umuhimu wa kuwajengea uwezo mabloga, akibainisha kuwa, "Wao wanabeba dhamana kubwa kutokana na wingi wao na wanatengeneza maudhui, na wengine si waandishi wa habari."

Aliongeza kuwa katika ulimwengu wa sasa wa teknolojia na akili bandia (AI), vyanzo vya habari vinavyotegemewa zaidi si mitandao ya kijamii, bali maandishi yanayopatikana kwenye blogu na tovuti, hivyo kufanya uhitaji wa mafunzo kuwa mkubwa zaidi.

Bwana Msimbe alitumia fursa hiyo kupongeza uamuzi wa kuandaa kikao hicho muhimu cha wadau, akisema kuwa ni hatua inayostahili kuelekea uchaguzi wa haki na uwazi. Licha ya changamoto ya mada nyingi (tisa) kujadiliwa ndani ya siku moja, alipongeza mkutano huo na jinsi ulivyokwenda.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Ndugu Msigwa, aliiagiza Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kuandaa mafunzo hayo mapema iwezekanavyo.

Kauli hiyo ya serikali imetafsiriwa na wadau mbalimbali kama hatua ya kutambuliwa rasmi kwa mchango wa mabloga katika tasnia ya habari na katika mchakato wa kidemokrasia.

Chama cha Mabloga Tanzania (TBN) kina wanachama zaidi ya 200 waliotawanyika kote nchini na nchi za nje, hivyo mafunzo haya yatakuwa na athari kubwa katika kuhakikisha usambazaji wa habari sahihi, zenye vigezo vya kitaaluma, na zinazozingatia maadili ya uandishi wa habari wakati wa kipindi cha uchaguzi na baadae.

Mkutano huo ulifunguliwa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Dk Doto Biteko ambaye alitaka vyombo vya habari na vya usalama kuhakikisha Amani na kuvumiliana kuelekea katika uchaguzi huo.

Share:

SERIKALI YAJA NA MKAKATI WA KUWAWEZESHA WAZALISHAJI CHUMVI NCHINI




Published from Blogger Prime Android App



▪️Serikali kupunguza ada ya kodi ya pango kwa mwaka kwa Leseni ya chumvi

▪️Rais Samia apongezwa kwa kiwanda cha kusafisha chumvi Lindi

▪️Wazalishaji wa chumvi wafurahia kuanza kwa kodi ya zuio

▪️Serikali kudhibiti uingizaji wa chumvi kiholela nchini

*Dar es Salaam*

Katika kuwajengea uwezo wazalishaji wa chimvi nchini,Serikali imekuja na mikakati mbalimbali kufikia azma hiyo ikiwemo  upunguzaji wa  ada ya pango kwa mwaka ya leseni (Annual Rent) za uchimbaji mdogo wa chumvi nchini ili kusaidia kupunguza gharama za uzalishaji na kuchochea uzalishaji wa wingi wa chumvi nchini.

Hayo yamesemwa jana tarehe 15 Julai, 2025 na Waziri wa Madini, *Mheshimiwa Anthony Mavunde (Mb)* Jijini Dar es Salaam alipokuwa akifunga Kikao cha wadau wa sekta ndogo ya chumvi chini ya Chama cha Wazalishaji wa Chumvi Tanzania (TASPA).

"*Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan* ameendelea kutubeba sekta ya madini na wachimbaji kwa ujumla. Ni yeye aliyetuelekeza kusikiliza kilio chenu na kutatua changamoto zinazowakabili ili mnufaike na shughuli mnazofanya"

"Ametuelekeza Wizara ya Madini tuliridhie ombi lenu na kupunguza ada ya pango ya mwaka ya leseni ya uchimbaji mdogo kutoka Shilingi 45,000 mpaka Shilingi 20,000 kwa hekta, hili linakwenda kupunguza gharama za uzalishaji na kuongeza ubora wa chumvi ya mzalishaji mdogo" alieleza Mhe. Mavunde.

Aidha, *Waziri Mavunde* alibainisha kuwa hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali ikiwemo udhibiti wa chumvi inayoingizwa kutoka nje ya nchi, zimepelekea bei ya chumvi ghafi kuongezeka na hivyo kuwanufaisha zaidi wazalishaji wadogo wa chumvi nchini.

Uanzishwaji wa kodi ya zuio ya asilimia mbili (2%) kwenye mauzo ya chumvi ghafi kwa wazalishaji wenye leseni za PML imekuwa ni neema na manufaa kwao badala ya utaratibu wa awali wa kufanyiwa makadirio ya kodi ya mapato, ambao ulikuwa ni kero kubwa kwa wazalishaji wadogo.

Katika hatua nyingine, Mhe. Mavunde alieleza kuwa Kiwanda cha kuzalisha chumvi cha STAMICO kipo hatua za mwisho, na kuagiza Shirika hilo kuhakikisha kabla ya mwezi wa Agosti kuisha kiwe kimekamilika na kuanza uzalishaji wa chumvi ili kupanua wigo wa soko la chumvi ya wazalishaji wadogo.

Awali, akitoa taarifa ya utendaji wa Taasisi yao, Mwenyekiti wa Chama cha Wazalishaji wa Chumvi Tanzania (TASPA), *Bi. Hawa Ghasia* aliishukuru Serikali kwa kushughulikia changamoto zilizokuwa zinaikabili sekta ndogo ya chumvi nchini ambazo zimepelekea bei ya chumvi kupanda na kuwanufaisha zaidi wazalisha chumvi nchini.
Share:

MAENDELEO YA TRILIONI 5.6 YABADILI SURA YA MWANZA




Published from Blogger Prime Android App



Na Joyce Kasiki,Dodoma


MKOA wa Mwanza umeendelea kung’ara kimaendeleo baada ya kupokea zaidi ya Shilingi trilioni 5.6 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kijamii na kiuchumi kuanzia Novemba 2020 hadi Aprili 2025.

Akizungumza jana jijini Dodoma kuhusu mafanikio ya Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan Mkuu wa mkoa huo Said Mtanda alisema fedha hizo zimetumika katika sekta muhimu zikiwemo afya, elimu, maji, miundombinu, usafirishaji, uwezeshaji wa wananchi kiuchumi pamoja na kuimarisha sekta ya utalii na biashara, na hivyo kuongeza ubora wa huduma kwa wananchi.

Afya na Elimu zilivyoimarika

Alisema,katika kipindi hicho, Serikali imetoa jumla ya Shilingi bilioni  63.2 kwa ajili ya kuboresha sekta ya afya na shilingi bilioni 196.8 kwa ajili ya kuboresha sekta ya elimu. 

Mtanda alisema Uboreshaji wa miundombinu ya shule na vituo vya afya umesaidia kupunguza msongamano wa wanafunzi madarasani, kurahisisha upatikanaji wa huduma za afya na kuongeza ari ya walimu na wanafunzi shuleni.

Aidha, ujenzi wa madarasa, nyumba za walimu na vituo vya afya umechangia kupunguza umbali kwa wanafunzi na wagonjwa wanaotafuta huduma muhimu, hali iliyoboresha kwa kiasi kikubwa ustawi wa wananchi.

Huduma ya maji ntafikia vyuo,vijiji na majumbani

Katika eneo hilo alisema,moka umepiga   hatua kubwa ambapo jumla ya Shilingi bilioni 264.8 zimetumika kuongeza upatikanaji wa maji mijini na vijijini. 

"Takwimu zinaonesha huduma ya maji mijini imeongezeka kutoka asilimia 57 mwaka 2020 hadi asilimia 85 mwaka 2025, huku vijijini ikiongezeka hadi asilimia 77.8."alisema na kuongeza kuwa 

"Mradi mkubwa wa ujenzi wa chanzo na kituo cha kutibu maji cha Butimba umegharimu Shilingi bilioni 71.6 na kuzalisha lita milioni 48 za maji kwa siku."

Alisema mradi huo unatarajiwa kupunguza tatizo la uhaba wa maji katika maeneo ya Nyegezi, Mkolani, Igoma, Buhongwa na Kisesa.

Share:

Serikali yazindua mafunzo ya afya moja (ECHO)




Published from Blogger Prime Android App




NA. MWANDISHI WETU – DAR ES SALAAM

SERIKALI imeanzisha mafunzo kwa njia ya mtandao ya Afya moja (ECHO) ili kuwajengea uwezo watoa huduma wa kada za afya ya binadamu, wanyama na mazingira kwa ngazi zote.

Hayo yamebainishwa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu Dk.Jim Yonazi wakati wa uzinduzi wa mafunzo hayo tarehe 15 Julai, 2025 katika Kituo cha kurushia Mafunzo kwa njia ya mtandao (ECHO HUB) kilichopo katika jengo la Idara ya Utafiti na Mafunzo Hospitali ya Taifa Muhimbili Jijini Dar es Salaam.

Amesema Serikali inaendelea kukabiliana na majanga na dharula zenye athari kwa afya ya binadamu, wanyama na mazingira hivyo imeona umuhimu wa kuwezesha wataalamu wake kuelewa kwa kina dhana ya Afya Moja.

“Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Wizara za Kisekta na mradi wa USAID Usalama wa Afya Duniani unaotekelezwa na Shirika la CIHEB Tanzania, imeanzisha mafunzo ya mtandao ya Afya moja (ECHO) ili kujenga uwezo kwa watoa huduma wa kada za afya ya binadamu, wanyama na mazingira kwa ngazi zote,”amesema Dkt. Yonazi.

Aliongeza kuwa; “Naomba niwahamasishe viongozi na watumishi kutoka sekta mbalimbali kushiriki katika vipindi hivi. Wataalamu wabobezi watawasilisha mada mbalimbali zitakazojenga uwezo wetu katika kuzuia, kujiandaa na kukabiliana na magonjwa ya mlipuko kwa binadamu na wanyama, visumbufu vya mazao, usugu wa vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa, usalama wa chakula.

Awali akieleza lengo la uzinduzi wa mafunzo hayo Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Brigedia Generali Hosea Ndagala amesema,Mafunzo haya yanayolenga katika kuongeza ufanisi kwa wataalam katika kushughulikia magonjwa ya kizoonotiki, usugu wa vimelea dhidi ya dawa (AMR), hatari za kibailojia, usalama wa chakula na magonjwa yasiyoambukizwa ambayo ni maeneo muhimu yenye changamoto na yanapewa kipaumbele katika Sekta ya Afya nchini Tanzania.

Alifafanua kuwa, Mafunzo haya yatawahusu wataalamu wa Sekta ya Afya moja, Afya, mazingira, mifuko na uvuvi.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Idara ya Huduma za Afya na Lishe Ofisi ya Rais-TAMISEMI Bi. Suzanne Nchalla  amesema mpango huo utasaidia watoa huduma ngazi ya msingi kupata uelewa wa Dhana ya Afya Moja na wakati wa utoaji huduma.

Amesema OR- TAMISEMI itashirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu katika kuhakikisha watumishi wa afya ya msingi wanashiriki kikamilifu katika mafunzo hayo.

“Tutawasimamia na kuwakumbusha viongozi wa Halmashauri kuhakikisha wanashiriki vipindi vilivyopangwa ili kupata matokeo chanya na kutimiza azma la mpango huu,”amesema Bi.Suzanne.

Naye Mwakilishi wa Mganga Mkuu wa Serikali Dkt.Otilia Gowelle alisema Wizara ya Afya inatambua umuhimu wa mashirikiano ya wadau na sekta mbalimbali katika kujiandaa pamoja na kukabiliana na matishio ya mara kwa mara ya magonjwa ya mlipuko pamoja na matukio yenye athari kwa afya ya binadamu. 

“Kwa kuzingatia umuhimu wa mafunzo haya, Wizara imekwisha fanya uhamasishaji na itaendelea kuhakikisha wataalam wengi zaidi wanashiriki mafunzo haya wakiwemo wauguzi, madaktari, wafamasia, maafisa afya, wataalam wa maabara na wengineo waliopo katika vituo vya kutolea huduma na maeneo mengine mahsusi” alisisitiza Dkt. Gowelle.

Aliongezea kuwa Wizara ya Afya imekuwa mshiriki na mnufaika mkuu wa ushirikiano uliopo kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu na kuahidi kuendelea kutoa ushirikiano kila inapohitajika.

=MWISHO=
Share:

DCEA:Hali ya dawa za kulevya nchini yazidi kuimarika,wanaotangaza ,kuhamasisha dawa za kulevya kukiona



Published from Blogger Prime Android App



Na Joyce Kasiki, DAR ES SALAAM

KAMISHNA Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), Aretas  Lyimo, amesema hali ya dawa za kulevya nchini Tanzania inaendelea kuimarika, huku matumizi na upatikanaji wa dawa hizo ukipungua kwa kiasi kikubwa kufuatia operesheni endelevu za Mamlaka hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba yanayoendelea jijini Dar es Salaam, Kamishna Lyimo alisema dawa aina ya heroin na cocaine zimepungua kwa kiwango kikubwa na sasa hazipatikani kwa urahisi hata katika vijiwe ambavyo awali vilikuwa vimeathirika zaidi.

“Hali hii ni matokeo ya juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali, ikiwemo kuwapeleka waraibu waliokuwa wameathirika katika vituo vya tiba kwa ajili ya kupata matibabu, ambayo yanatolewa bure kote nchini,” alisema Kamishna Jenerali Lyimo.

Aidha , Kamishna Jenerali Lyimo alisema Mamlaka hiyo imeendelea kutoa elimu kwa wananchi wanaofika kwenye Banda lao na kupewa Elimu kuhusu aina mbalimbali za dawa za kulevya pamoja na athari zake, sambamba na kuwaeleza wananchi kuhusu sheria zinazohusiana na matumizi, usambazaji na biashara ya dawa hizo haramu.

Aidha, alieleza kuwa DCEA ipo katika operesheni maalum ya kutoa elimu katika ngazi zote za elimu  kutoka shule za msingi, sekondari hadi vyuo kwa lengo la kuwakinga vijana na vishawishi vya kujiingiza kwenye matumizi au biashara ya dawa za kulevya.

“Lengo letu ni kuhakikisha kuwa ndani ya kipindi kifupi, tatizo la dawa za kulevya linatokomezwa kabisa nchini, na kila mwananchi anakuwa na uelewa wa kutosha juu ya madhara na athari za dawa hizo,” alisema.

Kamishna Jenerali Lyimo alisisitiza dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kuhakikisha kuwa wananchi wanakuwa na afya bora ili washiriki kikamilifu katika ujenzi wa uchumi wa Taifa.

Akitangaza msimamo mkali wa Serikali, alisema wale wote wanaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya hawatasalimika huku akisema hakuna namna watakuwa salama.

 “Mkono wa chuma utawafikia, na pumzi ya moto itawaelekea.”alisisitiza

Vilevile, aliwaonya watu wote wanaotangaza, kusifia au kuhamasisha matumizi ya dawa za kulevya kupitia mavazi, nyimbo au njia nyingine yoyote, kwamba hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.

Aidha  alitumia fursa hiyo kuwataka wazazi na walezi kuhakikisha wanawalinda watoto wao na kuwafundisha madhara ya dawa za kulevya, ili kujenga kizazi bora na kuimarisha uchumi wa Taifa kwa msingi wa rasilimali watu wenye afya na maadili.

Maonesho ya 49 ya Sabasaba yanaendelea kuvutia maelfu ya wananchi, huku DCEA ikiendelea kutumia jukwaa hilo kutoa elimu, hamasa na kuchukua hatua madhubuti dhidi ya biashara haramu ya dawa za kulevya nchini.
Share:

Mfumo Mpya wa Kudhibiti Umeme Nyumbani Watengenezwa na Wanafunzi wa NIT




Published from Blogger Prime Android App


 

Na Joyce Kasiki,Dar es Salaam

 

WANAFUNZI  wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) wameibuka na ubunifu wa kipekee kwa kutengeneza mfumo wa kisasa wa kudhibiti matumizi ya umeme majumbani, unaotumia teknolojia ya mawasiliano bila waya. 

 

Mfumo huo, uliopewa jina la Smart Home ulioneshwa kwa mara ya kwanza kwenye Maonyesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa yanayoendelea jijini Dar es Salaam.

 

Akizungumza wakati wa maonyesho hayo, Sayuni Haule, mwalimu wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), alisema kuwa mfumo huo umetengenezwa na wanafunzi wake kama sehemu ya mazoezi ya vitendo yanayolenga kutafsiri elimu ya darasani kwenda kwenye maisha halisi.

 

 Alisema kuwa mfumo huo ni mfano wa awali (prototype) unaoonesha jinsi teknolojia rahisi inaweza kutatua changamoto za kila siku za matumizi ya nishati majumbani.

 

“Kwa kutumia mfumo huu, mtu anaweza kuwasha au kuzima taa, feni na vifaa vingine vya umeme akiwa mbali na nyumbani kwa kutumia teknolojia ya mawasiliano isiyotumia waya,” alisema Mwalimu Haule,

 

“Mfano, mtu anaweza kuwa kazini au safarini na akagundua kuwa alisahau kuzima taa  kwa kutumia mfumo huu, anaweza kuzima taa hizo kwa kutuma ujumbe mfupi wa maandishi (SMS) bila ya kurudi nyumbani.”

 

Mwalimu Haule aliongeza kuwa mfumo huu unaleta urahisi  kwa watumiaji kwa kuwa unamwezesha mtu kuwa na udhibiti wa vifaa vya umeme popote alipo lakini pia ni msaada mkubwa kwa watu wenye ulemavu wa viungo kwani huwapa uwezo wa kuendesha mifumo ya nyumbani bila kulazimika kwenda moja kwa moja kwenye swichi.

 

Mbali na kuongeza urahisi,  amesema mfumo huu pia unasaidia kudhibiti matumizi ya umeme na kupunguza gharama. “Kwa mfano, unaweza ‘kufunga’ (lock) mfumo fulani wa umeme ambao hautaki utumike kwa muda husika,umeme utakuwepo lakini hautatumika hadi ufungue tena mfumo huo,” aliongeza.

 

Mradi huu unaonesha uwezo mkubwa wa wanafunzi wa NIT katika kuoanisha elimu na mahitaji halisi ya jamii. ni ishara njema kwa mustakabali wa teknolojia ya ndani ya nchi na inatoa matumaini ya maendeleo ya kiteknolojia yanayoendana na mazingira ya Kitanzania






Share:

FCC yatoa elimu ya ushindani wa kibiashara, Yazindua 'Clinic' ya Biashara kwa ushauri wa faragha



Published from Blogger Prime Android App


Na Joyce Kasiki,DAR ES SALAAM

MAMLAKA  ya Udhibiti wa Ushindani wa Kibiashara (FCC) imetumia fursa ya maonesho ya biashara kufikisha elimu kwa wadau wa sekta ya biashara huku ikizindua 'clinic' maalum ya kutoa ushauri wa faragha kwa wafanyabiashara kuhusu masuala ya ushindani na ulinzi wa walaji.

Akizungumza katika maonesho hayo, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Hadija Ngasongwa, alisema kuwa jukwaa hilo limewawezesha kufikia zaidi ya washiriki 3,500 kutoka sekta mbalimbali kwa lengo la kuhamasisha ushindani wenye tija na kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini.

“FCC imeanzisha clinic ya biashara ili kutoa nafasi kwa wafanyabiashara hasa wadogo na wa kati  kupata maarifa sahihi kuhusu sheria za ushindani na haki za walaji, kwa faragha na usiri unaohitajika,” alisema Bi. Ngasongwa.

Aliongeza kuwa pamoja na kuelimisha umma, FCC inaendelea kufuatilia mwenendo wa soko na kudhibiti bidhaa bandia ambazo si tu zinahatarisha afya za walaji, bali pia zinaharibu ushindani halali katika biashara.

Ngasongwa alieleza kuwa Serikali kupitia FCC imejenga mazingira rafiki ya kufanyia biashara, hali ambayo inaendelea kuwavutia wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi.

 “Sheria zetu ni rafiki kwa wawekezaji, na tunajivunia kwamba Serikali imeimarisha zaidi mazingira ya biashara, jambo linalochochea ukuaji wa uchumi na uwekezaji,” alisisitiza

Alifafanua kuwa FCC inaendelea kufanya tafiti za soko zenye lengo la kuhakikisha uwiano wa ushindani unazingatiwa, pamoja na kusaidia biashara ndogo kukua hadi kufikia viwango vya juu vya ushindani.

“Dhamira yetu ni kuhakikisha kuwa siyo tu wawekezaji wa nje wanafaidika na mazingira mazuri ya biashara, bali pia wajasiriamali wa ndani wanapata nafasi ya kukuza mitaji yao kupitia ushindani wa haki,” alieleza

Maonesho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kubadilishana uzoefu kati ya wadau wa biashara na taasisi mbalimbali, huku FCC ikichukua hatua za makusudi kuwa karibu zaidi na wafanyabiashara kwa njia ya ushauri wa moja kwa moja na elimu ya kisheria.

Share:

REA yawataka watanzania kuachana na dhana potofu kuhusu gharama za nishati safi ya kupikia



Published from Blogger Prime Android App

Published from Blogger Prime Android App

Published from Blogger Prime Android App

Published from Blogger Prime Android App



Na Joyce Kasiki,DAR ES SALAAM

 WAKALA  wa Nishati Vijijini (REA) umewahimiza Watanzania kote nchini kuondokana na mtazamo potofu kwamba matumizi ya nishati safi ya kupikia ni gharama kubwa ukilinganisha na kuni au mkaa, akisisitiza kuwa teknolojia ya kisasa imepunguza sana gharama hizo.

Rai hiyo imetolewa na Mkurugenzi wa Umeme Vijijini kutoka REA, Mhandisi Jones Olotu, wakati wa Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba) yanayoendelea jijini Dar es Salaam, katika banda la REA.

“Kumekuwepo na dhana kwamba kutumia nishati safi ya kupikia kama vile umeme ni gharama kubwa ikilinganishwa na kutumia kuni au mkaa. Hii si kweli. Teknolojia imebadilika sana sasa; kuna majiko ya kisasa yanayotumia umeme kwa kiwango kidogo sana,” alisema Mhandisi Olotu.

Aliwataka wananchi kutembelea banda la REA ili kujionea kwa macho jinsi teknolojia hizo zinavyofanya kazi na kuona jinsi upishi kwa kutumia nishati safi unavyowezekana bila kupoteza ladha ya chakula, huku muda wa kupika ukiwa mfupi zaidi.

Akizungumzia juhudi za REA katika kuhamasisha na kuwawezesha waendelezaji wa teknolojia za nishati safi ya kupikia, Mhandisi Olotu alieleza kuwa lengo ni kuwawezesha Watanzania kubadili mtindo wa maisha na kulinda afya zao pamoja na mazingira.

Kwa mujibu wa takwimu kutoka Wizara ya Afya, watu takribani 33,000 hufariki kila mwaka kutokana na athari za matumizi ya nishati chafu ya kupikia. Mhandisi Olotu alisisitiza kuwa REA ni miongoni mwa wadau wakuu wanaojitahidi kupunguza idadi hiyo kwa kutoa elimu na kuwapatia wananchi mbinu mbadala salama.

“Dhamira yetu ni kuachana kabisa na matumizi ya kuni na mkaa, lakini tunatambua kuwa mabadiliko haya hayawezi kufanyika kwa mara moja. Ndiyo maana tumekuwa tukisambaza majiko ya kisasa yanayotumia kiasi kidogo cha mkaa au kuni kama njia ya mpito,” alieleza.

Katika hatua za awali, REA imeanza kusambaza majiko ya gesi yenye mitungi ya kilo 6. Hadi sasa, jumla ya mitungi 3,255 pamoja na vichomeo vyake vimegawiwa katika kila wilaya Tanzania Bara kwa ruzuku ya asilimia 50, huku zoezi hilo likiendelea.

“Tunalenga kumwezesha kila Mtanzania kuhama kutoka kwenye matumizi ya nishati hatarishi kwenda kwenye matumizi ya nishati safi ya kupikia. Kwa wale wanaohitaji muda kubadilika, tumeanzisha suluhisho la mpito kwa kutumia teknolojia ya majiko yanayotumia mkaa kidogo,” aliongeza.

Aidha, alieleza kuwa REA inatekeleza agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, la kuzitaka taasisi zinazolisha watu zaidi ya 100 kutumia nishati safi ya kupikia.

“Tumeanza utekelezaji katika taasisi mbalimbali, zikiwemo Jeshi la Magereza. Mpaka sasa, maeneo 211 yameshafikiwa yakiwemo magereza 129, kambi 47, ofisi za mikoa 26, pamoja na nyumba za watumishi, vyuo, shule na hospitali,” alisema.

Nishati safi zinazotumika katika taasisi hizo ni pamoja na bayogesi, gesi ya mitungi (LPG), gesi asilia, mkaa kutoka makaa ya mawe, pamoja na mashine za kutengeneza mkaa mbadala. Vilevile, REA imewajengea uwezo Maafisa wa Magereza 280 kuhusu matumizi bora ya nishati safi.

Kwa ujumla, REA inaendelea kutoa elimu na kuwezesha upatikanaji wa teknolojia ya kisasa ili kuhakikisha Watanzania wengi zaidi wanahama kutoka matumizi ya nishati chafu kuelekea kwenye mfumo wa upishi salama, rafiki kwa afya na mazingira.


.


Share:

*SADC: SEKTA YA NISHATI IWE KICHOCHEO CHA KUIUNGANISHA AFRIKA KUJENGA UCHUMI*



Published from Blogger Prime Android App



📌 *Yasisitiza utekelezaji wa miradi ya kipaumbele ya Nishati*

📌 *Kapinga ataka SADC kuweka dhamira thabiti na mikakati madhubuti ya utekelezaji wa Ajenda ya Nishati Safi ya Kupikia*

Mawaziri wanaoshughulikia masuala ya Nishati na Maji wa Nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wametaka Sekta ya Nishati kuwa kichocheo cha kuiunganisha Afrika katika kujenga uchumi wake.

Wamesema hayo leo Julai 4, 2025  wakati wakihitimisha mkutano wa SADC jijini Harare nchini Zimbabwe ambao ulilenga kuimarisha na kujadili masuala mbalimbali yatakayowezesha mtangamano wa Kikanda katika sekta za nishati na maji.

Akizungumza wakati akihitimisha mkutano huo, Waziri wa Nishati na Maendeleo ya Umeme wa Zimbabwe, Mhe. Dkt. July Moyo, ameitaka jumuiya hiyo ya SADC kuipa kipaumbele sekta ya nishati na maji ili kuifanya kuwa na tija kwa wananchi katika kukuza uchumi wao kwa kuwa nishati  ni chanzo kikubwa cha maendeleo. 

Aidha, ameipongeza Tanzania kwa kuandaa na kuwa mwenyeji wa kufanikisha Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Nishati Afrika wa Misheni 300 (M300) ambao ulifanyika kwa mafanikio. Pia, Dkt. Moyo amezishukuru Nchi wanachama zilizohudhuria katika mkutano huo muhimu uliofanyika jijini Dar es Salaam. 

Kwa upande wake, Waziri wa Nishati wa Malawi, Mhe. Ibrahim Matola ameitaka SADC kuhakikisha inaiendeleza miradi yote ya kipaumbele katika jumuiya ili kuifanya sekta ya nishati kuwa kimbilio katika kujenga uchumi wa nchi zao. 

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga ameitaka SADC kuhakikisha inakuwa na mikakati madhubuti ya utekekezaji wa maazimio mbalimbali wanayofikia  katika makongamano ya umoja huo ili yawe na tija kwa wananchi na taifa kwa ujumla na kuifanya sekta ya nishati kuwa chachu na mkombozi ndani ya SADC. 

Kuhusu utekelezaji wa nishati safi ya kupikia katika jumuiya hiyo, Mhe. Kapinga ameitaka SADC kuweka dhamira thabiti na mikakati madhubuti ya utekelezaji wa ajenda ya nishati safi ya kupikia ili kuwafikia watu wengi zaidi katika SADC. 

Mkutano huo uliohitimishwa leo, umehudhuliwa na Balozi wa Tanzania nchini Zimbabwe, Mhe. Suzan Kaganda, Wataalam mbalimbali kutoka Wizara ya Nishati akiwemo Kamishna Msaidizi wa Maendeleo ya Umeme, Mha. Styden Rwebangila, Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mha. Hassan Saidy, Mkurugenzi wa  Mipango na Uwekezaji (TPDC), Derick Moshi, Mkurugenzi wa Mifumo ya Udhibiti Umeme (TANESCO) , Mha. Deogratius Mariwa, Mkurugenzi wa Udhibiti Uchumi (EWURA), Msafiri Mtepa na  Wataalam kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Share:

Waziri Ridhiwani Atoa Wito kwa Vijana Kuchangamkia Fursa Zilizopo

Published from Blogger Prime Android App


 
Na Mwandishi Wetu - Dar es Salaam.

 
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Ridhiwani Kikwete ametoa wito kwa vijana kuchangamkia fursa mbalimbali zilizopo ikiwemo mikopo na mifuko mbalimbali ya uwezeshaji
Wananchi kiuchumi.


Mhe. Kikwete ametoa wito huo wakati alipotembelea Banda Jumuishi la Ofisi ya Waziri Mkuuu lililopo katika Maonesho ya Biashara ya Kimataifa SABASABA, leo tarehe 04 Julai, 2025 Jijini Dar es Salaam.
 

“Serikali imeendelea kutenga fedha kuhakikisha makundi mbalimbali yananufaika, kwa mfano kupitia maelekezo ya kisera kwenye Sheria ya PPRA imeelekezwa asilimia 30  ya manunuzi yote ya umma ipelekwe katika kusaidia makundi ya Vijana, akinamama na Wenye Ulemavu," ameeleza Mhe. Ridhiwani.

 
Aidha, ameongeza kuwa upo mfuko maalumu wa kusaidia watu wenye ulemavu,  lakini pia upo mfuko wa vijana na mfuko wa uwezeshaji wananchi kiuchumi, hivyo mifuko yote hiyo kama vijana na  wananchi  wakiikimbilia hakika vilio vya uwezeshaji havitaweza kutokea.
 
 
Pia, Mhe. Kikwete amewata Waandishi wa Habari, Watumishi wa Umma na wadau mbalimbali kuzidi kupaza sauti juu ya uwepo wa mifuko hiyo na faida zake kwa wananchi .


Vilevile, ameelekeza Idara na Taasisi za serikali ziendelee kutoa elimu kwa wananchi hususani Vijana ili waweze kujua fursa za mikopo na uwezeshaji wananchi zilizopo.


“Maelekezo yetu ni kwamba Idara zetu zote, taasisi zetu zote waendelee kuhakikisha kwamba elimu inakuwa ndiyo kipaumbele kwa sababu serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mambo yaliyofanyika ni uwezeshaji wa kifedha, uwezeshaji wa watu, uwezeshaji wa kielimu, tumefanya mambo mengi sana na tumehakikisha watu wetu wanapatiwa elimu ili waweze kujinusuru katika maeneo haya” amebainisha Mhe. Ridhiwani.


Mbali na hayo Mhe. Ridhiwani amewataka Watanzania na hasa kipindi hiki ambacho nchi inaelekea katika Uchaguzi Mkuu kulinda amani iliyopo ili kuweza kufikia lengo lililokusudiwa.


=MWISHO=

Share:

PSPTB yatangaza Usajili wa Mitihani ya 31,wadau waombwa kujisajili mapema


Published from Blogger Prime Android App


Published from Blogger Prime Android App


Published from Blogger Prime Android App


Picha zote zinaonesha wajumne wa Bodi ya PSPTB wakiwa katika picha ya pamoja kwenye maonyesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara kwenye banda la PSPTB 




Na Mwandishi wetu

BODI ya Wataalam wa Ununuzi na Ugavi (PSPTB) imetangaza rasmi kuanza kwa usajili wa mitihani yake ya kitaaluma ya 31, itakayofanyika kuanzia Agosti 25 hadi Agosti 29, 2025, katika kituo maalum kilichopo jijini Dodoma.

Akizungumza Leo Julai 4,2025 na waandishi wa habari  katika Maonyesho ya Kimataifa ya 49 ya  Biashara yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam , Mkurugenzi Mtendaji wa PSPTB,  Godfred Mbanyi, amewahimiza   waombaji wote wenye sifa  kujisajili kupitia mfumo wa mtandaoni unaopatikana kwa anuani https://registration.psptb.go.tz.

"Tunapenda kuwafahamisha wadau wetu kuwa usajili wa mitihani ya 31 umefunguliwa rasmi,tunawasihi wale wote wanaokusudia kufanya mitihani hii wajisajili mapema kabla ya tarehe ya mwisho ya kupokea maombi ambayo ni Agosti 15, 2025," amesema Mbanyi.

Kwa mujibu wa Mbanyi , kwa sasa mitihani hiyo itafanyika katika kituo kimoja tu Dodoma  ili kuimarisha uratibu na kuhakikisha usimamizi bora wa mitihani hiyo muhimu kwa taaluma ya ununuzi na ugavi nchini.

Aidha Mkurugenzi huyo,   amewaasa wazazi na walezi kushiriki kikamilifu kwa kuwasomesha na kuwafadhili watoto wao walioko kwenye nyanja ya ununuzi na ugavi, kwa kuhakikisha wanalipiwa ada za usajili wa mitihani hiyo.

"Natoa rai kwa wazazi na walezi kuchangia katika maendeleo ya taaluma hii kwa kuwalipia ada watoto wao,hatua hiyo ni uwekezaji muhimu katika kukuza rasilimali watu yenye weledi na uadilifu," aliongeza.

Aidha, Mkurugenzi huyo amewataka wadau wote wa PSPTB nchini kote kuendelea kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na uzalendo kwa manufaa ya Taifa, akisema kuwa taaluma ya ununuzi na ugavi ni mhimili muhimu katika usimamizi wa rasilimali za umma na sekta binafsi.

Kwa mujibu wa PSPTB, mitihani hiyo ya kitaaluma ni sehemu ya mfumo wa kutoa ithibati kwa wataalamu wa ununuzi na ugavi, ambao wana mchango mkubwa katika kudhibiti matumizi ya fedha na kuhakikisha thamani halisi ya manunuzi kwa taasisi mbalimbali nchini.



Share:

Theme Support

Need our help to upload or customize this blogger template? Contact me with details about the theme customization you need.

Labels

Blog Archive

Recent Posts

Unordered List

  • Lorem ipsum dolor sit amet, consectetuer adipiscing elit.
  • Aliquam tincidunt mauris eu risus.
  • Vestibulum auctor dapibus neque.

Pages

Theme Support

Need our help to upload or customize this blogger template? Contact me with details about the theme customization you need.